Mahakama Kuu ya
Mtwara imeondoa mahakamani shauri la kupinga matumizi ya Kanuni za
Maudhui ya Kimtandao (Online Content Regulation) lililofunguliwa na Kituo cha
Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) na wenzake dhidi ya Waziri wa Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo.
Mbali na LHRC
wengine waliopeleka zuio hilo ni Tanzania Human Rights Defenders (THRD); Baraza
la Habari Tanzania(MCT) na Jamii Media; Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake
Tanzania (TAMWA ); na Jukwaa la Wahariri (TEF).
Kanuni hizo
zilipaswa zianze kutumika Mei 5 lakini mahakama hiyo ikaweka zuio la muda Mei
4, baada ya kuwasilishwa kwa shauri la kupinga mahakamani hapo.
Kesi hiyo namba
12/2018 ilisomwa jana Mei 28 mbele ya Jaji Mfawidhi, Dk Fauz Twaib na ilipangwa
kutolewa uamuzi juu ya mapingamizi matatu yaliyowasilishwa na upande wa
Serikali.
Akitoa uamuzi huo
jana, Jaji Dk Twaib alisema mahakama hiyo imekubali pingamizi moja kati ya
matatu yaliyowasilishwa; kwamba mashirika yaliyopeleka kesi mahakamani hapo
hayana maslahi ya kutosha kwa maana ya kufungua shauri hilo na kwamba
hawakuonyesha namna moja kwa moja yatakavyoguswa na kanuni hizo.
Hivyo, mahakama
iliondoa shauri hilo lakini inatoa nafasi kwa mashirika hayo kama yatahitaji
kupeleka shauri lingine kama watajidhihirisha wana nafasi ya kufanya hivyo.
Na Zania Miraji
Comments
Post a Comment